tangazo

tangazo

Saturday, April 19, 2014

KAMPUNI MBALI ZA BIASHARA ZASAJILIWA KATIKA KIPINDI CHA ROBO TATU YA MWAKA WA FEDHA 2013/2014

Jumla ya kampuni 160, alama za biashara 430, majina ya biashara 280, jumuiya za kiraia 67 na nyaraka 583 zimesajiliwa katika kipindi cha robo tatu ya mwaka wa fedha 2013/2014.
 
Akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji Mpangokazi wa Wizara ya Katiba na Sheria kwa kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014 jana Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Assaa Ahmad Rashid alieleza pia kuwa katika kipindi hicho Wizara imesajili vizazi 27,445 kote nchini.
 
Alibainisha kuwa kati ya vizazi hivyo 13,742 ni wanaume na 13,703 ni wanawake huku vifo vilivyosajiliwa vikiwa ni 1,648 kati yake wanawake ni 760 na wanaume 888.
 
Katika kikao hicho Katibu Mkuu huyo alibainisha kuwa katika kuimarisha utoaji huduma za Zakka na Wakfu Wizara katika kipindi hicho imeendelea na jitihada za kuelimisha waumini kuhusu masuala hayo ambapo mikutano 24 iliyokusanya wadau mbalimbali ilifanyika na miongozo ya zakka, mirathi na Wakfu iligawiwa Unguja na Pemba pamoja na kutoa vipindi vya elimu kwa njia ya redio na televisheni.
 
Katika hatua nyingine taarifa hiyo ilieleza kuwa Wizara imo mbioni kukiimarisha Kituo cha Utafiti na Mafunzo ya Sheria Zanzibar ambapo hivi karibuni kinatarajiwa kupata hati ya utambulisho(accreditation) ili kuanza kutoa mafunzo ya sheria katika ngazi ya cheti na Stashahada kuanzia mwezi Julai mwaka huu.
Kwa upande wa hakimiliki taarifa hiyo ilieleza kuwa Wizara kwa mara ya kwanza imeweza kugawa mirahaba kwa wasanii na wabunifu 726 ambapo jumla ya shilingi milioni 36 ziligawiwa. Katika kipindi hicho Wizara imeweza pia kusimamia mapito ya Sheria ya Hakimiliki.
 
Kuhusu ukusanyaji wa mapato katika Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa hadi mwisho wa robo tatu ya mwaka wa fedha Wizara imekusanya shilingi milioni 345.1 ikiwa ni sawa na asilimia 79 ya lengo la kukusanya shilingi milioni 435.
 
Katika kikao hicho kilichofanyika Ikulu Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi DK. Ali Mohamed Shein amezitaka Wizara na Taasisi za Serikali zilizo na jukumu la kukusanya mapato kuongeza juhudi ili Serikali iweze kupata mapato zaidi ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake.
 
Alibainisha kuwa mwenendo wa ukusanyanji mapato kwa upande wa Bodi ya Mapato Zanzibar- ZRB na Mamlaka ya Mapato Tanzania-TRA unakwenda vizuri kwa makusanyo kuongezeka mwaka hadi mwaka lakini alisisitiza kuwa wizara na Taasisi nyingine zinapaswa kuiga mfano wa taasisi hizo.
 
Mhe Rais alizikumbusha Wizara kuzingatia utaratibu wa Bangokitita kwa kuwa ni utaratibu endelevu unaokwenda sambamba na mfumo wa ukusanyaji mapato na matumizi ya Serikali pamoja na utekelezaji wa kazi za Serikali ambao unategemea bajeti iliyopangwa.
 
Katika kikao hicho alihimiza uwekaji wa kumbukumbu za Serikali kwa kuanzisha na kuimarisha maktaba katika wizara na taasisi za serikali ili kutoa fursa kwa watumishi kuongeza taaluma zao na kujifunza mambo mbali yanayofanyika katika Wizara na taasisi pamoja na duniani kwa jumla.
 
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee.   

DK SHEIN AGIZA KUFANYIKA UTAFITI WA KINA KUJUA TATIZO LA UHABA WA WALIMU WA SAYANSI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kufanya utafiti wa kina kujua hali halisi ya tatizo la uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi na hesabati na kutengeneza mpango mkakati wa kulimaliza kabisa tatizo hilo.
 
Dk. Shein amezungumza hayo wakati wa mjadala wa Taarifa ya Utekelezaji wa Mpangokazi wa Wizara hiyo kwa kipindi cha Julai 2013 na Machi 2014 ikiwa ni mfululizo wa vikao vya kujadili taarifa za utendaji kazi za Wizara za Serikali vinavyofanyika Ikulu.
 
Alisema ili kukabiliana na tatizo hilo ni lazima utafiti wa kina ufanyike kuelewa mahitaji halisi ya walimu hao kwa kuainisha waliopo hivi sasa na walimu watarajiwa walioko vyuoni ili mpango wa kuongeza walimu hao kukidhi mahitajiutayarishwe na kutekelezwa.
 
Kwa kufanya hivyo alieleza kuwa tatizo hilo litaweza kutafutiwa suluhisho la kudumu kwa kushirikiana na taasisi za elimu nchini ikiwemo Chuo Kikuu cha Zanzibar –SUZA.
 
Katika kikao hicho Dk. Shein aliitaka Wizara hiyo kutoa elimu zaidi kuhusu mabadiliko yaliyofanywa na Serikali kupitia Baraza la Mitihani Tanzania-NECTA ya madaraja ya ufaulu ili kuepusha upotoshaji.
 
“ni muhimu jamii ikaelimishwa vya kutosha kuhusu mabadiliko hayo ili kusiwe na fursa kwa baadhi ya watu kulipotoshwa kwa makusudi suala hili” Dk. Shein alisisitiza.
 
Kuhusu kuimairisha huduma za maktaba Mhe Rais alisisitiza suala la maktaba kupatiwa majarida muhimu ya kitaaluma hasa yale ya sayansi ambayo ni muhimu katika kuwasaidia wanafunzi na watafiti katika fani zao.
 
Aliihimiza wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuharakisha maandalizi ya sheria ya kuanzisha Taasisi ya Elimu nchini ili chombo hicho muhimu katika ukuzaji wa elimu nchini kiweze kutekeleza majukumu yake.
 
Katika kikao hicho Dk. Shein alikumbusha na kusisitiza umuhimu wa michezo maskulini na kuielekeza Wizara, kwa sasa ambapo walimu wenye taaluma ya michezo ni wachache, kuweka mpango wa kuwa na walimu angalau wawili wa kuhamasisha michezo ambao watapewa mafunzo.
 
Wakati   huo huo Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali imekamilisha ujenzi wa madarasa 118 yaliyoanzishwa na wananchi pamoja na kuzifanyia ukarabati skuli saba za msingi na nyumba nne za walimu.
 
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpangokazi wa Wizara hiyo jana Katibu Mkuu Bi Mwanaidi S. Abdalla alieleza kuwa kati ya madarasa hayo 66 yako Unguja na yako 52 Pemba.
 
Sambamba na ujenzi huo alisema kuwa wizara imeweza kutengeneza na kuyapatia madarasa hayo mapya jumla ya madawati 1,800, viti 144 na meza 144. Aidha Wizara hiyo alisema ilipokea msaada wa madawati 100 toka kwa Benki ya NMB.
 
Kwa upande wa vitabu Bi Mwanaidi alieleza kuwa katika kipindi hicho jumla ya nakala 142,210 za vitabu vya wanafunzi na nakala za miongozo 3,820 ya walimu ilichapishwa.
 
Alifafanua kuwa vitabu na miongozo hiyo ambayo ni ya madarasa ya kwanza hadi la nne ya masomo ya Sayansi, Sayansi Jamii, Kiswahili na Kingereza ilianza kusambazwa maskulini mwezi Januari mwaka huu.
 
Katibu Mkuu huyo alieleza kuwa wizara yake imeelekeza nguvu zake katika kukabiliana na changamoto zinazoikabili sekta ya elimu nchini kwa kuweka vipaumbele katika maeneo ya ongezeko la utoaji elimu na kuimarisha kiwango cha elimu inayotolewa.
 
Kwa minajli hiyo Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu ya Juu ya Oman inaandaa programu ya mafunzo kazini kwa walimu wanaofundisha masomo ya sayansi, hesabati na lugha ya kingereza katika ngazi ya sekondari ili kuwajengea uwezo zaidi walimu hao kumudu majukumu yao.
 
Pamoja na programu hiyo Bi Mwanaidi alisema mafunzo mengine ya aina mbali mbali kwa walimu yanafanyika katika vituo vya Ualimu ili kuongeza ufanisi kazini.
 
Sambamba na hatua hizo taarifa hiyo ilieleza kuwa Wizara tayari  imeshakamilisha Rasimu ya Sheria ya Uanzishwaji wa Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Elimu ikiwa ni sehemu ya jitihda za kuhakikisha ubora wa kiwango cha elimu nchini.
 
Bi Mwanaidi alikieleza kikao hicho kuwa katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014 idara hiyo ya Ukaguzi wa Elimu ilikamilisha ukaguzi wa skuli 293 sawa na asilimia 86 ya lengo la mwaka.
 
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee. 

Wednesday, April 9, 2014

ccm wakanusha kutaka kuchakachua rasimu ya pili ya katiba


ZANZIBAR.

 

CHAMA CHA MAPINDUZI KIMEKANUSHA VIKALI KUWA KINA LENGO KUCHAKACHUA RASIMU YAPILI YA KATIBA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA.

 

AKIZUNGUMZA NA WATENDAJI WA MIKOA NA MAKATIBU WA WILAYA WA CCM  LEO HUKO KATIKA OFISI KUU YA CCM KISIWANDUI MJINI ZANZIBAR NAIBU KATIBU MKUU WA CCM ZANZIBAR NDUGU VUAI ALI VUAI  AMESEMA KUWA TAARIFA ZILIZOTOLEWA NA VYOMBO VYA KHABARI KUHUSU SUALA HILO HAZINA UKWELI WOWOTE.

 

AMEVITAKA VYOMBO VYA KHABARI KUACHA TABIA YAKUTOA TAARIFA ZISIZO NA UKWELI  NA KUIPOTOSHA JAMII KUWA CCM INA MPANGO WAKUZIPINGA KANUNI ZA BUNGE AMBAZO ZIMEWEKWA KWA LENGO LAKUENDESHA VIKAO VYA BUNGE MAALUM LA KATIBA.

 

AIDHA VUAI AMESEMA KUWA CHAMA CHA MAPINDUZI NI SEHEMU YA WANANCHI HIVYO  MAPENDEKEZO WATAKAYOYATOA BUNGENI YATATOKANA NA MSIMAMO WA CHAMA HICHO.

 

AMEVITAKA VYAMA VYA UPINZANI  KUFAHAMU KUWA BUNGE MAALUM LA KATIBA LIPO KWA MASLAHI YA WATANZANIA WOTE NA SI WAZANZIBARI PEKEE.

mchango wa kikwete barani afrika waonekana


dar-es-salaam.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, dr Jakaya Mrisho Kikwete amechaguliwa kuwa Kiongozi Mwenye Mchango Mkubwa katika Maendeleo Barani Afrika kwa mwaka 2013 .

 

kwa mujibu wa taaarifa iliyotolewa na kurugenzi ya mawasiliano ikulu mjini dar-es-salaam Heshima hiyo kwa Rais Kikwete imetolewa na jarida maarufu la kimataifa la African Leadership Magazine Group na Tuzo ya heshima hiyo itatolewa leo jioni  katika sherehe iliyopangwa kufanyika  katika Hoteli ya St. Regis mjini Washington, D.C ikiwa ni pamoja na chakula cha jioni.

 

Tuzo hiyo itapokelewa kwa niaba ya Rais Kikwete na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, ambaye tayari amewasili mjini Washington kwa sherehe hiyo kubwa.

 

Tuzo hiyo ya heshima kubwa hutolewa kwa viongozi wa Afrika ambao hutoa mchango mkubwa zaidi wa kiuchumi na kijamii kila mwaka kwa watu wao na imetolewa kwa Rais Kikwete kwa mwelekeo wake usiokuwa wa kawaida na wenye mafanikio makubwa katika  masuala ya utawala bora.

 

Jarida hilo limesema kuwa ukweli wa hali hiyo bora ya utawala bora chini ya  uongozi wa Rais Kikwete umeendelea kumiminiwa sifa kimataifa na leo umeifanya Tanzania kuwa nchi ya kuigwa mfano kama kituo cha uhakika cha uwezeshaji kutokana na mageuzi makubwa yaliyofanywa katika sera na mifumo ya uchumi.

 

Jarida hilo linasema kuwa Rais Kikwete alikuwa chaguo kubwa na la kwanza la wasomaji wa Jarida hilo ambao walipiga kura kupitia njia mbali mbali za mawasiliano za jarida hilo.

mitambo ya redio ya kiislam zanzibar yaungua


ZANZIBAR.

studio  namba tatu ya kituo cha radio ya kiislam ya al-noor fm kilichopo katika maeneo ya masjid swahaba mtoni kidatu zanzibar imeungua moto usiku wakuamkia leo baada yakutokea khitilafu za umeme.

akizungumza na radio adhana fm mkurugenzi wa radio hiyo al-ustadh muhammed suleiman  amesema kuwa mtangazaji wa zamu aliyekuwepo studioni hapo jana usiku abuubakar fakih hamad amekatika mguu wakulia na kuumia mkono baada yakujirusha kutoka ghorofa ya kwanza ya jengo la kituo hicho wakati wakujaribu kujinusuru na moto huo.

ameongeza kuwa mtangazaji huyo akupata athari yoyote yakuungua moto huo na hivi sasa anaendelea na matibabu katika hospitali kuu ya mnazi mmoja mjini zanzibar.

akivitaja vifaa vilivyovyongua baada yakutokea moto huo ustadh muhammed amesema kuwa ni pamoja na mtambo wa stl  ambao unatumika  kwaajili yakusafirishia matangazo kutoka katika studio hiyo hadi katika eneo lakurushia matangazo la masingini wilaya ya magharibi unguja,mixer kubwa aina ya yamaha na fanicha kadhaa zilizokuwemo ndani.

ustadh muhammed amesema kuwa katika kuonyesha utukufu wa kitabu kitukufu cha qur-an kilichonusurika katika chumba kilichongua ni misahafu iliyokuwemo  pekee.

aidha mkurugenzi huyo amefafanua kuwa hadi sasa hasara iliyopatikana kutokana na moto huo haijafahamika.

amesema kuwa juhudi zakurejesha matangazo hayo zinaendelea  hivyo amewaomba waskilizaji kuwa wastahamilivu katika kipindi hiki kifupi ambacho matangazo ya radio hiyo hayatokuwa hewani .

kituo cha radio al-noor fm kinatangaza kupitia mhz 93.03  unguja na 92.06 pemba kimekuwa kikiungua mara kadhaa kutokana na khitilafu za umeme.

 

Friday, April 4, 2014

SERIKALI YA SMZ YA AHIDI KUTORUDI NYUMA KUTEKELEZA MIRADI YA MAENDELEO LICHA YA CHANGAMOTO MBALI MBALI


ZANZIBAR

 

SERIKALI IMESEMA HAITARUDI NYUMA KUTEKELEZA AZMA YAKE YA KULIENDELEZA ENEO LA MICHENZANI MJINI UNGUJA HIVYO AMELITAKA SHIRIKA LA HIFADHI YA JAMII ZANZIBAR-ZSSF AMBALO NDILO LINALOTEKELEZA MRADI HUO KUHAKIKISHA KUWA LINAKABILIANA NA CHANGAMOTO ZOTE ZINAZOTOJITOKEZA KATIKA UTEKELEZAJI WAKE.

RAIS WA ZANZIBAR A,BAYE PIA NI MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI DK. ALI MOHAMED SHEIN AMESEMA HAYO WAKATI ALIPOKUWA AKIZUNGUMZA NA VIONGOZI NA WATENDAJI WA SHIRIKA HILO PAMOJA NA VIONGOZI WA SERIKALI WAKATI ALIPOFANYA ZIARA KUKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA MNARA WA KUMBUKUMBU YA MAADHIMISHO YA MIAKA 50 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR.

KATIKA MAELEZO YAKE KWA MHE RAIS MKURUGENZI MKUU WA ZSSF BWANA ABDULWAKIL HAJI HAFIDH ALIELEZA KUWA MRADI HUO WA KULIENDELEZA ENEO LA MICHENZANI UNAKABILIWA NA TATIZO LA UMILIKI WA BAADHI YA MAENEO LIKIWEMO LA MAKONTENA HIVYO AKAIOMBA SERIKALI KUSAIDIA KUYATATUA.

ALIUTAKA UONGOZI WA ZSSF KUFANYA MAZUNGUMZO NA WAFANYA BIASHARA WALIOPO KATIKA ENEO LA MAKONTENA JUU YA NAMNA YA KUPISHA UJENZI KATIKA ENEO HILO NA KUELEZA KUWA ANAAMINI KWAMBA WATAAFIKI KWANI NAO WANGEPENDA KUFANYA SHUGHULI ZAO KATIKA MAENEO MAZURI YENYE KUVUTIA.

ALIWAELEZA VIONGOZI WALIOKUWEPO KATIKA ENEO HILO KUWA AMEAMUA KUTEMBELEA MRADI HUO ILI KUJIONEA MWENYEWE MAENDELEO YA UTEKELEZAJI WAKE KWA KUWA AMEKUWA AKISIKIA NAMNA UJENZI HUO UNAVYOENDELEA KUTOKA KWA WATU MBALIMBALI.

AWALI MKURUGENZI MKUU WA ZSSF BWANA ABDULWAKIL HAJI HAFIDH ALIMUELEZA MHE RAIS KUWA UJENZI WA MNARA HUO WENYE MITA 33 UNAENDELEA VIZURI NA UMESHAFIKIA MITA 21.

ALIELEZA KUWA CHANGAMOTO KUBWA KATIKA KUTEKELEZA MRADI WA KULIBORESHA ENEO LA MICHENZANI KWA KUJENGA MAJENGO YA BIASHARA NA MAKAAZI NI NAMNA YA KUWAHAMISHA KWA MUDA WAFANYABIASHARA WA MAKONTENA PAMOJA NA UTATA WA UMILIKI WA BAADHI YA MAENEO HAYO KUTOTAMBULIWA NA SERIKALI WAKATI WATU WANAYAMILIKI.

WAKATI HUO HUO RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI DK. ALI MOHAMED SHEIN AMEITAKA ZSSF KUZINGATIA KWA MAKINI UENDESHAJI WA MRADI WA KIWANJA CHA KUFURAHISHIA WATOTO ILI KUHAKIKISHA KUWA KIWANJA HICHO KINAENDESHWA KIBIASHARA NA KIWEZE KUREJESHA FEDHA ZILIZOWEKEZWA.

AKIZUNGUMZA MARA BAADA YA KUTEMBELEA ENEO LA KARIAKOO LINALOJENGWA KIWANJA HICHO DK SHEIN AMELITAKA SHIRIKA HILO KUZINGATIA PIA MASUALA YA USALAMA WA WATU WATAKAOTUMIA KIWANJA HICHO HASA MILANGO YA KUINGILIA NA KUTOKEA.

AKITOA MAELEZO YAKE KWA MHE RAIS, MKURUGENZI MKUU WA ZSSF BWANA ABDULWAKIL HAJI HAFIDH ALIELEZA KUWA UTEKELEZAJI WA MRADI HUO UMESHAVUKA ASILIMIA 50 NA KINATARAJIWA KUKAMILIKA NA KUANZA KUTUMIKA IFIKAPO MWEZI JULAI MWAKA HUU.

HATA HIVYO ALIFAFANUA KUWA SUALA LA KUCHELEWA KUWASILI VIFAA VYA UJENZI NDIO LIMESABABISHA MRADI KUTOKWENDA KWA KASI ILIYOKUSUDIWA LAKINI ALIELEZA KUWA VIFAA HIVYO VINATARAJIWA KUWASILI NCHINI HIVI KARIBUNI.

ALIFAFANUA KUWA KIWANJA HICHO KITAKUWA NA PEMBEA 12 PAMOJA NA HUDUMA NYINGINE KAMA MADUKA 61, SEHEMU ZA KUFANYIA MAONESHO PAMOJA NA HARUSI ,VYOO 30 PAMOJA NA SEHEMU KUBWA YA KUEGESHA MAGARI.

RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI ALITEMBELEA PIA SKULI YA SEKONDARI YA LUMUMBA ILIYOPO MJINI UNGUJA AMBAKO ALIKAGUA MAZINGIRA YA SKULI HIYO KONGWE HUMU NCHINI.

Tuesday, April 1, 2014

DOKTA SHEIN AKUTANA NA WAZIRI CHIKAWE


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe ofisini kwake Ikulu.

 

Waziri Chikawe ambaye alifuatana na Naibu wake Bwana Pereira Ame Silima alifika Ikulu kujitambulisha rasmi kufuatia mabadiliko ya Baraza la Mawaziri yaliyofanywa na Rais Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete mwezi Januari mwaka huu.

 

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimpongeza Waziri Chikawe na Naibu Waziri Silima kwa kukubali uteuzi wa kushika uongozi wa Wizara hiyo yenye majukumu mazito na muhimu ya ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

 

Alimueleza waziri huyo kuwa Taasisi za Wizara yake Zanzibar zinafanya vizuri na kuzipongeza taasisi hizo kwa ushirikiano wake na utekelezaji mzuri wa majukumu yao.

 

Hata hivyo alieleza kuwa pamoja na taasisi hizo, ikiwemo Jeshi la Polisi kukabiliwa na changamoto kadhaa lakini watendaji wake wamekuwa wakionesha ujasiri na kuliletea sifa jeshi hilo.

 

Alitoa pongezi maalum kwa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa-NIDA kwa kazi nzuri ambayo imekuwa ikiifanya tangu zoezi la uandikishaji wa vitambulisho hivyo ilipoanza hapa Zanzibar.

 

Dk. Shein aliukumbusha uongozi wa Wizara hiyo ya Mambo ya Ndani ya Nchi wakiwemo Waziri na Naibu Waziri kuweka utaratibu maalum wa kutembelea taasisi zake zilizoko Unguja na Pemba mara kwa mara ili kuangalia utendaji na mazingira ya utendaji kazi ya taasisi hizo.

 

Katika mazungumzo hayo ambayo yalihudhuriwa pia na Mkurugenzi Mkuu wa NIDA Bwana Dickson Maimu na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA Zanzibar Bwana Vuai Mussa Suleiman, Dk. Shein aliitaka Wizara hiyo pamoja na mafanikio iliyoyapata kuongeza juhudi na kuongeza ufanisi katika kutekeleza majukumu yake.

 

Wakati huo huo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mathias Chikawe katika mazungumzo hayo alimwambia Mhe Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuwa Wizara yake imejidhatiti katika kuimarisha utendaji kazi wa wizara na taasisi zake kwa kubuni mbinu na mikakati ambayo inaendana na mazingira ya sasa.

 

Aliongeza kuwa wizara  na taasisi zake zinatekeleza majukumu yake na ulinzi wa raia na mali zao na kuwa jitihada zinafanywa kuzipatia nyenzo taasisi zinazohusika ili kuongeza ufanisi katika kazi.